AFISA MWANDIKISHAJI JIMBO LA IRAMBA MAGHARIBI AWATAKA WAENDESHA VIFAA VYA BVR NA WAANDIKISHAJI WASAIDIZI KUFANYA KAZI KWA WELEDI ILI KUFANIKISHA ZOEZI LA UBORESHAJI WA DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA AWAMU YA PILI
Afisa Mwandikishaji wa Jimbo la Iramba Magharibi Bi. Magreth Segu Mei 14, 2025 amefungua rasmi mafunzo ya siku moja kwa Waendesha Vifaa vya BVR (Biometric Voter Registration) pamoja na Waandikishaji Wasaidizi ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya utekelezaji wa zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura awamu ya pili.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo Bi. Segu amewataka washiriki wa mafunzo kufanya kazi kwa weledi, bidii na kwa kujituma kwa kufuata Taratibu na Miongozo waliyofundishwa ili kuhakikisha zoezi hilo linafanyika kwa ufanisi.
"Inatarajiwa kuwa baada ya mafunzo haya mtaenda kufanya kazi kwa weledi, bidii na kwa kujituma kwa kufuata Taratibu na Miongozo mliyofundishwa...natarajia mtafanya zoezi hili kwa ufanisi ili kufanikisha zoezi hili la kitaifa" Amesema Bi Segu
Aidha ametoa wito kwa washiriki wa mafunzo hayo kuhakisha wanawahimiza Wananchi wenye sifa ili wajitokeze Kujiandikisha, kuhakiki na kuboresha taarifa zao ili kupata Haki yao ya kikatiba itakayo wawezesha kushiriki katika kuchangua viongozi wao.
Mafunzo hayo kwa watu 125 ni sehemu ya maandalizi kuelekea zoezi la Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura awamu ya pili, linalotarajiwa kufanyika kuanzia Mei 16 hadi 22, 2025 katika Jimbo la Iramba Magharibi.
Zoezi la uboreshaji wa daftari linatarajiwa kuwapa nafasi wananchi ambao hawakujiandikisha awali, waliopoteza kadi au waliohama maeneo yao ya awali, kujiandikisha upya au kufanya marekebisho muhimu ili waweze kushiriki kikamilifu katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu 2025.
Hata hivyo, zoezi la Uboreshaji Daftari la kudumu la wapiga kura awamu ya Pili litaenda sambamba na zoezi la Uwekaji Wazi wa Daftari la Awali la Wapiga Kura. Huku Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi ikisisitiza umuhimu wa Kila mwananchi kushiriki zoezi Hilo kilamilifu.
KIOMBOI, IRAMBA
Anuani ya Posta: P.O BOX 155. KIOMBOI-IRAMBA
Simu: 026 - 2532253
Simu: 026 - 2533001
Barua pepe: ded.irambadc@singida.go.tz
Copyright ©2017 Iramba District Council . All rights reserved.