DC MWENDA ATOA WITO KWA WALIMU WA SHULE ZA MSINGI KUIMARISHA UFUNDISHAJI KWA MADARASA YA MITIHANI
Singida, Mei 6, 2025
Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Yusuph Mwenda, amewahimiza walimu wa shule za msingi wilayani humo kufundisha kwa bidii madarasa yanayotarajia kufanya mitihani ya kitaifa, ili kuendeleza mwenendo chanya wa ufaulu wa wanafunzi katika wilaya hiyo.
Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa wilayani Iramba, Mwenda alisisitiza umuhimu wa kuendeleza mafanikio yaliyopatikana mwaka 2024 ambapo Halmashauri ya Wilaya ya Iramba ilishika nafasi ya 8 kitaifa katika shule zilizoongeza ufaulu wa darasa la saba nchini, ikiwa imeongeza ufaulu kwa asilimia13.
"Tunapaswa kuendeleza rekodi ya matokeo mazuri katika Wilaya yetu. Fundisheni kwa juhudi zote Madarasa yenye Mitihani ya Kitaifa ili mwaka huu pia tuendelee vunja rekodi ya kuongeza ufaulu pamoja na kupata matokeo mazuri." Amesema DC Mwenda
Katika ziara hiyo, DC Mwenda pia aliwapongeza wananchi wa Iramba kwa kujitolea nguvu kazi kusaidia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.
“Nawapongeza sana wananchi wa Iramba kwa moyo wenu wa kujitolea. Katika kila eneo nililopitia, nimekuta mwitikio mkubwa wa wananchi kushiriki kwenye shughuli za maendeleo. Hili ni jambo la kupongezwa sana na kujivunia,” aliongeza DC Mwenda.
Katika ziara hiyo, DC Mwenda alikagua miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa Wilayani Iramba ikiwemo: ujenzi wa ukamilishaji bweni la wasichana katika Shule ya Sekondari Kidaru (Thamani: Shilingi milioni 60), ujenzi wa matundu 10 ya vyoo Shule ya Msingi Kidaru (Shilingi milioni 17), ujenzi wa matundu 10 ya vyoo Shule ya Msingi Tyegelo (Shilingi milioni 17), ukamilishaji wa Kituo cha Afya Tyegelo (Shilingi milioni 150), ujenzi wa matundu 10 ya vyoo Shule ya Msingi Luono (Shilingi milioni 17), ujenzi wa Shule ya Msingi Nkokilangi (Shilingi milioni 250), ujenzi wa Zahanati ya Mseko (Shilingi milioni 250), mradi wa ufungaji wa mfumo wa gesi ya kupikia katika Shule ya Sekondari Shelui (Shilingi milioni 27.7).
DC Mwenda aliongozana na Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya, Wataalamu mbalimbali kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Iramba.
KIOMBOI, IRAMBA
Anuani ya Posta: P.O BOX 155. KIOMBOI-IRAMBA
Simu: 026 - 2532253
Simu: 026 - 2533001
Barua pepe: ded.irambadc@singida.go.tz
Copyright ©2017 Iramba District Council . All rights reserved.