Mkuu wa Wilaya ya Iramba Mkoani Singida Suleiman Yusuph Mwenda ametoa wito kwa walimu Wilayani Iramba kuendelea kufanya kazi kwa bidii na ubunifu ili kuendelea kuinua ufaulu wa wanafunzi Wilayani hapa.
Mwenda ameyasema hayo Desemba 8, 2025 alipokuwa akifunga kikao cha Tathmini ya Matokeo ya Mtihani wa Kuhitimu Elimu ya Msingi (PSLE 2025) kilichofanyika katika ukumbi mkubwa wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, na kuhudhuriwa na walimu wakuu wa shule za msingi, Maafisa elimu kata, Afisa Ajira Cosmas Cosmas kutoka Tume Ya Utumishi Wa Walimu (TSC) Wilaya na Mthibiti Ubora Mkuu wa Shule Wilaya Bi. Neema Makia.
"Niwaombe tuongeze nguvu, juhudi na ubunifu katika kazi zetu. Tuipende kazi hii ili kuendelea kufanikisha ongezeko la ufaulu Wilayani Iramba, pasiwe na uzembe eneo la kazi, ambao utatukwamisha." Amesema DC Mwenda
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba Michael Matomora aliwataka washiriki wa kikao hicho kutekeleza maazimio yote ya kikao hicho ili kuboresha zaidi sekta ya elimu. Pia, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya walimu katika kufanikisha malengo ya elimu wilayani Iramba.
Halmashauri ya Wilaya ya Iramba imepata ufaulu wa asilimia 79.6 mwaka 2025 sawa na ongezeko la aslimia 2.3 la mwaka 2024 lenye ufaulu wa asilimia 77.3 katika mtihani wa kuhitimu elimu ya msingi (darasa la saba). Ikumbukwe kwamba kuanzia mwaka 2023 hadi mwaka 2025 kumekuwa na ongezeko la ufaulu kwa asilimia 15.
KIOMBOI, IRAMBA
Postal Address: P.O BOX 155. KIOMBOI-IRAMBA
Telephone: 026 - 2532253
Mobile: 026 - 2533001
Email: ded.irambadc@singida.go.tz
Copyright ©2017 Iramba District Council . All rights reserved.