KAMATI YA AFYA YA MSINGI (PHC) IRAMBA YAJADILI MIKAKATI YA CHANJO YA POLIO SINDANO YA PILI
Iramba, Mei 9, 2025
Kamati ya Afya ya Msingi (PHC) ya Wilaya ya Iramba imekutana kujadili masuala mbalimbali ya afya, ikiwa ni pamoja na magonjwa ya mlipuko na mikakati ya chanjo kwa jamii. Mkutano huo ulifanyika katika ukumbi mdogo wa mikutano wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba na kuongozwa na Mkuu wa Wilaya, Mhe. Suleiman Yusuph Mwenda.
Miongoni mwa ajenda kuu zilizojadiliwa ni pamoja na kuanza rasmi kwa utoaji wa chanjo ya pili ya sindano ya POLIO kwa watoto. Kwa mujibu wa maelezo ya kamati hiyo, kuanzia Mei 1, 2025, watoto wanaofikisha umri wa miezi 9 watapatiwa chanjo ya pili ya sindano ya POLIO. Aidha, watoto wenye umri wa wiki 14 wataendelea kupokea chanjo kama ilivyopangwa awali.
Chanjo hiyo inapatikana katika vituo vyote vinavyotoa huduma za chanjo pamoja na maeneo yanayohudumiwa kupitia chanjo za mkoba ili kuhakikisha watoto wote wanapata huduma hiyo muhimu bila vikwazo.
Kamati hiyo imesisitiza umuhimu wa kutoa elimu kwa jamii na kufanya uhamasishaji katika makundi mbalimbali ili kuongeza mwitikio wa chanjo na kulinda afya ya jamii dhidi ya magonjwa ya mlipuko.
Mkutano huo ulihudhuriwa na wajumbe mbalimbali wa Kamati ya Afya ya Msingi kutoka ngazi tofauti, huku maazimio ya pamoja yakiwa ni kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa mikakati hiyo ya afya.
Wasilisho la chanjo hiyo ya sindano ya pili ya Polio limewasilishwa na mratibu wa chanjo wa Halmashauri Bw. Jackson Shillah.
KIOMBOI, IRAMBA
Anuani ya Posta: P.O BOX 155. KIOMBOI-IRAMBA
Simu: 026 - 2532253
Simu: 026 - 2533001
Barua pepe: ded.irambadc@singida.go.tz
Copyright ©2017 Iramba District Council . All rights reserved.