Kitengo cha Wagonjwa Mahututi (ICU) katika Hospitali ya Wilaya ya Iramba, kilichopo Old Kiomboi, kimeanza kutoa huduma kwa mafanikio makubwa baada ya Serikali ya Awamu ya Sita kutenga Shilingi milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa jengo jipya na ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa.
Uanzishwaji wa ICU hiyo umekuwa hatua muhimu katika kuboresha huduma za afya wilayani, ambapo huduma zilianza rasmi mwezi Oktoba 2024. Kuwepo kwa vifaa tiba vya kisasa, kama mashine ya umeme wa moyo (defibrillator) na vifaa vingine vya hali ya juu, kumewezesha hospitali kutoa huduma ambazo hapo awali zilipatikana tu katika hospitali za rufaa au za mikoa.
Nicodemus Dickson Nduche, mtaalamu wa huduma za dharura na wagonjwa mahututi, alisema kuwa uwekezaji huu umeleta mabadiliko makubwa katika utoaji wa huduma za afya wilayani.
*"Zamani huduma hizi zilikuwa zinapatikana katika hospitali kubwa pekee, lakini sasa wagonjwa wanapata matibabu hapa hapa wilayani. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutupatia fedha kwa ajili ya ujenzi wa jengo hili na ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa. Wagonjwa wanaridhika na huduma tunazotoa,"* alisema Nduche.
Tangu kuanzishwa kwa ICU hiyo, tayari wagonjwa 12 wamepokea matibabu, hatua inayoonyesha umuhimu wa uwekezaji huu katika kuokoa maisha. Uboreshaji huu wa huduma za afya unatarajiwa kupunguza rufaa za wagonjwa kwenda hospitali za mikoa na rufaa, na hivyo kuokoa muda na gharama kwa wananchi wa Iramba.
KIOMBOI, IRAMBA
Anuani ya Posta: P.O BOX 155. KIOMBOI-IRAMBA
Simu: 026 - 2532253
Simu: 026 - 2533001
Barua pepe: ded.irambadc@singida.go.tz
Copyright ©2017 Iramba District Council . All rights reserved.